September 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TARURA yasikitishwa na wanaohujumu miundombinu

Na Magesa Magesa,TimesMajira Online. Arusha

WAKALA wa Barabara za Mijini na Vijijini(TARURA) mkoani hapa, umeelezea kusikitishwa kwake na baadhi ya wananchi ambao wamekuwa wakihujumu
miundombinu ya barabara kwa kuiba kingo za madaraja na vyuma ambavyo vikimekwa alama za barabarani na kuviuza kama vyuma chakavu.

Mratibu wa TARURA Mkoa wa Arusha, Mhandisi Edward Amboka ameyasema hayo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya
changamoto mbalimbali zinazoikabili TARURA na kuwataka wanaojihusisha na vitendo hivyo kuacha mara moja.

‘’Hali hii licha ya kusababisha hasara na kutumia gharama kubwa kuvirejesha, pia imekuwa ikichangia madereva kuvunja sheria za usalama barabarani kutokana na kutokuwepo kwa alama hizo, jambo ambalo kwa kiasi kikubwa limekuwa likichangia ajali za mara kwa mara,” amesema.

Mhandisi Amboka ameiomba serikali kufanya ukaguzi wa kushtukiza wa mara kwa mara katika maeneo yote ya Mkoa wa Arusha, ambapo hufanyika biashara ya vyuma chakavu na kuwakamata watakaobainika kukutwa na vyuma hivyo vya barabarani, ili waweze kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Amesema changamoto nyingine wanayokumbana nayo ni uvamizi wa hifadhi za barabara, hususan maeneo ya vijijini, ikiwemo kufanya shughuli za kibinadamu pembezoni mwa barabara kama vile kufuga, kulima
na ujenzi wa majengo kwa ajili ya makazi na biashara.