September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kiongozi wa ACT Wazalendo, Zitto Kabwe,

RC Andengenye amjulia hali Zitto, wenzake hospitalini

Na Mwajabu Kigaza,TimesMajira,Online Kigoma

MKUU wa Mkoa wa Kigoma Kamishna wa Polisi, Thobias Andengenye, amemtembelea na kumjulia hali Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe na makada wenzake watano wa chama hicho aliopata nao ajali juzi wakati gari lake lilipopata ajali wakielekea kwenye kampeni.

Zito na makada hao wanapatiwa matibabu katika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Maweni.

Ajali hiyo iliyotokea katika Kata ya Kalya jana baada ya gari alilokuwa amepanda kugongwa na gari lingine kwa nyuma na kusababisha majeraha kwa wanasiasa hao.

Baada ya ajali hiyo Zitto na makada hao walipata huduma ya kwanza katika Kituo cha Afya Kalya na baadaye kuhamishiwa Hospitali ya Rufaa Mawenzi kwa uchunguzi zaidi. RC Ndengenye alimpa pole Zitto na makada hao na alitoa wito kwa madereva kuwa makini pindi wanapoendesha vyombo vya moto ili kuepusha ajali zisizokuwa za lazima barabarani.

Zitto amesema gari iliyowagonga kwa nyuma ni la mgombea ubunge Jimbo la Kigoma Kusini kwa tiketi ya ACT Wazalendo na kwamba ajali hiyo ilisababishwa na vumbi lililotanda barabarani.

“Kwa mujibu wa taarifa za wataalamu wa afya nimeambiwa kuwa bega langu la mkono wa kushoto lina tatizo ambapo kuna mfupa ambao umevunjika, lakini naendelea vizuri kwa sasa,” amesema Zitto

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Dkt. Saimon Chacha ameeleza kuwa huduma zinaendelea kutolewa kwa majeruhi wote na kuwa Zitto anatarijiwa kusafirishwa kwenda Dar es salaam kwa ajili ya matibabu pamoja na vipimo zaidi.

MWISHO