September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

5169 waanza kufanya mitihani Namtumbo

NA Yeremias Ngerangera,TimesMajira Oline,Namtumbo

WANAFUNZI 5169 wameanza mitihani yao ya kumaliza elimu ya msingi mwaka 2020 katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma huku kukiwa na jumla ya wavulana 2445 na jumla ya wasichana 2724.

Afisa elimu msingi wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo Protas Komba alisema jumla ya shule 108 ndizo zitafanya mitihani hiyo na shule 3 zimeanzishwa karibuni hazina wanafunzi wa darasa la saba.

Alizitaja shule zilizoanzishwa karibuni kuwa ni shule ya msingi PAX,shule ya msingi Miembeni pamoja na shule ya msingi ST.Nicolous ambapo kwa pamoja inazifanya Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo kuwa na jumla ya shule 111 na shule 108 pekee ndizo zinazohusika na ufanyaji wa mitihani ya darasa la saba kwa mwaka huu 2020.

Kwa mujibu wa Komba alidai mitihani imeanza na wanafunzi wote wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo wapo kwenye vyumba vya mitihani wakiendelea kufanya mitihani kwa kufuata sheria ,kanuni na taratbu za wizara .

Aidha mwalimu mkuu wa shule ya msingi Mwenge iliyopo Mamlaka ya Mji Mdogo wa Namtumbo Aidan Ndomba alisema mitihani inaendelea vyema katika shule yake ambayo inajumla ya wanafunzi watahiniwa 60 wasichana 30 na wavulana 30 na wote wapo kwenye chumba cha mtihani.

Hata hivyo mwalimu mkuu wa shule ya msingi Namtumbo Pambo Mahundi naye alidai anawatahiniwa 105 wanaofanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka huu 2020 kukiwa na jumla ya wasichana 64 na wavulana 41.

Evance Nachimbinya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo alisema kuwa mitihani ya kitaifa imeanza vyema katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo na mitihani hiyo inaendelea vizuri katika shule zote 108 zinazofanya mitihani hiyo.