September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ujenzi mradi wa stendi kutoa ajira 200

Na Judith Ferdinand,TimesMajira Online. Mwanza

MRADI wa ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi na malori unaondelea kujengwa Kata ya Nyamhongolo Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza, umetoa ajira zaidi ya 200 kwa watu wenye taaluma na wasiokuwa na taaluma, huku ukikamilika utasaidia kukuza uchumi na kupunguza changamoto ya ajira kwa wakazi wa Ilemela.

Mradi huo ambao utatumia sh. bilioni 28 mpaka kukamilika mbali na kutoa ajira, pia itatoa fursa kwa wafanyabiashara wadogo wadogo kufanya biashara na hivyo kufanya kipato cha wananchi kuongezeka na uchumi kukua.

Akizungumza wakati alipotembelea mradi huo wa ujenzi wa stendi hiyo, ikiwa ni sehemu ya kuona na kufuatilia namna utekelezaji wake unavyoendelea Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye pia ni mgombea Ubunge wa Jimbo la Ilemela kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Angeline Mabula amesema Serikali ya CCM kwa kipindi cha miaka mitano, imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ikiwemo stendi ya kisasa ambao umeweza kuajiri zaidi ya watu 200 wenye utaalamu na wasio na ujuzi rasmi.

Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye pia ni Mgombe Ubunge Jimbo la Ilemela kupitia CCM Dkt. Angeline Mabula (kulia) akisikiliza maelezo kutoka kwa Wasimamizi wa mradi wa ujenzi wa stendi ya kisasa ya malori na mabasi Nyamhongolo.

Amewahimiza wananchi wa kata hiyo, kutumia fursa ya uwepo wa mradi huo kujikwamua kiuchumi kwa kufanya biashara na kuanzisha miradi mingine ndani na jirani ya stendi, hivyo wajiandae kuwekeza pale utakapokamilika na wasiogope waombe vyumba vya kufanyia biashara.

“Nimefurahishwa na uwepo wa mkakati wa ujenzi wa eneo la kufanyia biashara wajasiriamali wadogo wadogo maarufu kama machinga jirani na stendi hii, jambo litakalosaidia kupunguza migogoro isiyokuwa ya lazima kama inayojitokeza maeneo mengi ya mijini, kutokana na kukosekana kwa maeneo rasmi ya wafanyabiashara hao,” amesema.