September 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Taasisi yaahidi kugawa miche ya mikorosho bure

Na Nathaniel Limu,TimesMajira Online. Singida

TAASISI ya Ant Desert Envirowment Scheme (ADESE) ya mkoani Singida, imeahidi kusaidia miche ya mikorosho na kuigawa bure kwa wakulima mkoani hapa, ili kila kaya inayojihusisha na kilimo cha zao hilo kuimarika kiuchumi.

Akizungumza na Majira mwishoni mwa wiki Mkurugenzi wa ADESE Mkoa wa Singida, Kitanto Saidi amesema kugawa miche mbalimbali bure ni mwendelezo wa asasi hiyo, ambayo imelenga zaidi kuhifadhi na kuboresha mazingira pia kuondoa uwezekano wa nchi kugeuka na kuwa jangwa.

Amesema katika kitalu chao, wameotesha miche ya kutosha ya kujenga uchumi ambayo ni na mikorosho na migunga inayotoa gundi.

“Ili mkulima aweze kupata miche hii ya mikorosho, mingunga au miche mingine ya aina mbalimbali ni lazima atuletee barua kutoka kwa Mtendaji wa Kijiji au Kata,” amesema na kuongeza;

“Barua hiyo itatuhalakishia sisi kwamba mhusika ana eneo la kutosha la, kuendeleza shamba la mikorosho au mimea mingine. Akitupa barua hiyo tutampatia fomu maalumu itakayoainisha miche anayotaka”.