September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt. Nchimbi azindua miradi iliyotekelezwa

Na John Mapepele,TimesMajira Online. Ikungi

MKUU wa Mkoa wa Singida, Dkt. Rehema Nchimbi juzi amezindua miongoni mwa miradi mikubwa iliyowahi kutekelezwa nchini, mradi wa pamoja baina ya Mashirika ya Kimataifa ya UN Women na UNFPA kupitia ufadhili wa Shirika la KOICA wa ‘Tuufikie usawa wa jinsia kupitia kuwawezesha wanawake na wasichana’.

Mradi huo utagharimu takribani sh. bilioni
11.5 za Kitanzania ambao utatekelezwa katika Wilaya ya Ikungi mkoani Singida na Msalala mkoani Shinyanga kwa kipindi cha miaka mitatu, kuanzia sasa.

Dkt. Nchimbi amesema lengo kuu la mradi huo ni
kuchangia katika kuwawezesha wanawake na wasichana kuwakwamua kiuchumi na kijamii katika Mikoa ya
Singida na Shinyanga, ili kufikia usawa wa kijinsia ambapo amewataka watendaji wote wa serikali ambao watatekeleza mradi huo kuwa makini kwenye utekelezaji wa mradi, ili malengo ya mradi huo yaweze kufikiwa.

Amesisitiza kuwa serikali, haitasita kuwachukulia hatua kali watendaji ambao kwa namna moja au nyingine, hawataendana na kasi ya utekelezaji wa miradi chini ya Serikali ya awamu ya tano
inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli, ambapo amesema mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ili kuwaletea wananchi maendeleo ya kweli.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa KOICA Tanzania, Jieun Mo, walengwa wasio wa moja kwa moja takribani wakazi 40,000 kutoka kwenye Wilaya za Ikungi na Msalala na walengwa wa moja kwa moja 2,350 wanawake na wasichana kutoka katika wilaya hizo, watanufaika na mradi huu ambapo pia wanaume na wanawake 6,000 wa Wilaya ya Ikungi, watanufaika kwenye eneo la muingiliano wa hati za ardhi.