September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri wa Kilimo, Josephat Hasunga

Hasunga apiga marufuku ‘makomandoo’ Mbozi

WAZIRI wa Kilimo, Japhet Hasunga amepiga marufuku utaratibu uliobuniwa na Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi wa kutumia makomandoo kwa lengo la kupunguza vifo vya vya akinamama na watoto wachanga kabla, wakati na baada ya kuzaliwa.

Amelazimika kupiga marufuku mpango huo uliozinduliwa Februari mwaka huu, baada ya kupigiwa kelele na wananchi wakiwemo wanasiasa wa vyama vya upinzani, ambapo inadaiwa kuwa watu hao wanaoitwa makomandoo huwatoza faini kati ya sh. 30,000 hadi sh. 50,000 wajawazito ambao hushindwa kwenda kliniki.

Akizungumza na wananchi kwenye mikutano ya hadhara ya kampeni, ametangaza kupiga marufuku kikundi hicho kwa kuwa kinadhalilisha wanawake.

“Kuanzia sasa hakuna cha komandoo wala nini, kwa hiyo tunachotaka mwananchi akiwa mjamzito aende kliniki kwa wataalamu, unakwenda kumwambia komandoo una mimba je ana utaalamu, kasomea au anajua hata mimba zinakuweje,” amehoji Hasunga.

Hasunga ambaye anagombea Ubunge Jimbo la Vwawa, amesema kinachosikitisha zaidi ni kwamba mama mjamzito hata akienda kliniki anaambiwa ni lazima awe na barua kutoka kwa komandoo.

Amesema mambo hayo hayawezi kukubalika yaendelee katika jimbo lake na kwamba kuanzia, sasa kikundi hicho kiache mara moja kufanya vitendo vya kuwatoza wananchi faini.