March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mhandisi Ntemi ahoji upatikanaji gari zimamoto Katoro

Na Joyce Kasiki, Dodoma

MBUNGE wa Jimbo la Katoro, Mhandisi Kija  Ntemi, ameihoji Serikali kuhusu  upatikanaji wa huduma za Jeshi la Zimamoto na Uokoaji katika jimbo la Katoro mkoani Geita.

Akiuliza swali Bungeni jijini Dodoma Mbinhe huyo Swali hilo lililenga kujua ni lini Serikali itapeleka gari la zimamoto Katoro ili kuwezesha utoaji wa huduma za haraka pindi dharura zinapotokea.

“Je ni lini Serikali itapeleka gari la zimamoto Katoro ili kuwezesha utoaji wa huduma za haraka pindi dharura zinapotokea.”

Akijibu swali hilo Naibu  Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Ayoub Mohamed Mahmoud  ameeleza kuwa, Serikali inaendelea kuchukua hatua madhubuti za kuliimarisha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini.

Amesisitiza kuwa jitihada hizo ni sehemu ya mkakati mpana wa kuhakikisha usalama wa wananchi na mali zao unalindwa kwa ufanisi zaidi.

Naibu Waziri alifafanua kuwa Serikali imekuwa ikilipa kipaumbele suala la vitendea kazi kwa jeshi hilo, ikiwemo ununuzi wa magari ya kisasa ya kuzima moto na uokoaji hatua  inayolenga kuongeza uwezo wa jeshi hilo kufika maeneo ya matukio kwa wakati na kutoa msaada unaohitajika haraka.

“Serikali ilitangaza kuwa Jimbo la Katoro tayari limepatiwa gari moja jipya la zimamoto na uokoaji aina ya IVECO. Gari hilo ni la kisasa na linatarajiwa kuboresha kwa kiasi kikubwa utoaji wa huduma za zimamoto katika eneo hilo.”alisema Naobu Waziri huyo

Kwa mujibu wa majibu wa Naibu Waziri Mahmoud, gari hilo kwa sasa lipo Mkoani Dar es Salaam likikamilishiwa taratibu za mwisho kabla ya kusafirishwa.

Naibu Waziri aliongeza kuwa gari la zimamoto linatarajiwa kufika Mkoani Geita  09 Februari, 2026 huku akisema  kuwa, ujio wa gari hilo utaimarisha usalama wa wananchi wa Katoro na maeneo ya jirani, hasa katika kukabiliana na majanga ya moto na dharura nyingine.