March 8, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

TMA yatoa utabiri wa mwelekeo wa mvua za msimu

Na Penina Malundo ,Timesmajira

MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imetoa utabiri wa  mwelekeo wa mvua za msimu mwaka 2025 hadi Aprili 2026 huku ikitangaza  uwepo wa  mvua  zitakazokuwa kwa kiwango cha wastani hadi chini ya wastani.

Kutokana na uchache wa mvua hizo za msimu,TMA imetaja athari zitakazoweza  kujitokeza kipindi hicho ni pamoja na  upungu wa unyevunyevu, kupungua kwa kina cha maji katika baadhi ya vyanzo vya maji yanayotumika kwa shughuli za binadamu na mifugo, upungufu wa malisho ya wanyamapori na  kuathiri usafirishaji. 

Akitangaza mwelekeo huo wa mvua za msimu  jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Ladislaus Chang’a, amesema mvua hizo zinatarajiwa kuanza Novemba 2025 hadi Aprili 2026 kwa baadhi ya maeneo zitachelewa kuanza.

Amesema mvua hizo zinatarajia  kuanza wiki ya tatu hadi ya nne ya Oktoba mwaka huu kwa ukanda wa Magharibi katika mikoa ya Kigoma, Singida na Tabora.

Amesema mvua hizi zinatarajiwa kuisha wiki ya nne ya Aprili au wiki ya kwanza ya Mei mwakani, ambapo kiwango cha mvua kinatarajiwa kuwa chini ya wastani hadi wastani.

“Kwa Kanda ya Kati inayojumuisha mikoa ya Dodoma na Singida mvua zinatarajiwa kuanza wiki ya kwanza hadi ya pili ya mwezi Desemba na kuisha wiki ya tatu hadi ya nne ya mwezi Aprili mwakani na kiwango cha mvua kitakuwa chini ya wastani hadi wastani.

Amesema katika  Mifumo ya utabiri imeonesha uwepo wa mvua za chini ya wastani hadi wastani kwa mikoa ya Kigoma, Tabora, Katavi, Singida na Dodoma. 

“Hata hivyo, mvua za wastani hadi chini ya

wastani zinatarajiwa katika mikoa ya Njombe, Iringa, Mbeya, Songwe, Rukwa, Ruvuma,

Mtwara na Lindi pamoja na maeneo ya kusini mwa mkoa wa Morogoro.

“Pamoja na uchache wa mvua hizi pia zitachelewa kuanza kusini mwa Mkoa wa Morogoro huko tunatarajia zitaanza kati ya wiki ya pili na ya tatu ya Novemba. Kwa ile mikoa minguni mvua hizi zitaanza wiki ya tatu na ya nne ya Oktoba, 2025 na kuisha wiki ya nne ya Aprili 2026,” amesema Dkt Chang’a.

“Kwa upande wa Nyanda za Juu Kusini Magharibi, mvua zinatarajiwa kuanza wiki ya pili hadi ya tatu ya Novemba na kuisha wiki ya nne ya Aprili hadi wiki ya kwanza ya mwezi Mei mwakani, kiwango cha mvua kitakuwa chini ya wastani hadi wastani.”amesema.

Aidha amezitaka mamlaka mbalimbali kuchukua hatua kwa kuwaeleza wakulima aina ya mazao yanayohimili ukame na kuhifadhi maji kadiri iwezekanavyo.