September 22, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt. Biteko akoshwa na SGR

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Dotto Biteko akiwasalimia na kuwasikiliza abiria mbalimbali waliosafiri naye katika treni ya mwendokasi maarufu ‘SGR’ kutokea Dar es Salaam mpaka Jijini Dodoma leo Septemba 12, 2024

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dkt. Ditto Biteko amesema safari za treni za Reli ya Kisasa (SGR) zinazotumia umeme kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma ni ushahidi kuwa Tanzania ina umeme wa kutosha.

Dkt. Biteko ameyasema hayo leo Septemba 12, 2024 baada ya kuwasili Jijini Dodoma akitokea Dar es Salaam kwa kutumia usafiri wa treni ya mwendo kasi (SGR) kwa mara ya kwanza.

“Safari za treni ya umeme ya SGR ni ushahidi mwingine kuwa nchi ya Tanzania ina umeme wa kutosha, ni ushahidi mwingine kwamba nishati ya umeme ikipatikana ya uhakika inafungua fursa mbalimbali za kiuchumi, viwanda mbalimbali vinajengwa na kongani za viwanda kuongezaka”, amesema Dkt. Biteko

Katika kuhakikisha umeme unatosheleza Dkt. Biteko amesema Wizara ya Nishati kazi yake ni kuhakikisha umeme unakuwepo wa kutosha wakati wote na kuongeza kuwa wizara inasimamia ujenzi wa laini nyingine ya kuutoa umeme kutoka Chalinze kwenda Dodoma kwa laini kubwa zaidi na kutoa umeme kutoka Bwawa la kuzalisha umeme la Julius Nyerere kwenda Dodoma baadae Singida, arusha hadi Mwanza.

Hata hivyo, Dkt. Biteko amefurahishwa na usafiri huo wa treni ya mwendokasi maarufu SGR kuwa ni waharaka na umeendelea kuvutia watu wengi kutumia, hivyo tutahakikisha umeme unaendelea kuwa wa kutosha ili watanzania waendelea kutumia huduma hiyo.