September 22, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Maadhimisho ya siku ya mtoto wa kike kufanyika Dodoma

Na Mwandishi wetu, Timesmajira

TAFITI  zinaonyesha kuwa asilimia 44.4 ya wanafunzi wa Shule za  Sekondari hawana uelewa wa   Demokrasia  huku asilimia 85.5 hawajawahi kushiriki wala  kushirikishwa katika vikao rasmi vya shule vinavyofanya uamuzi.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam,Mmoja wa wasichana Viongozi kutoka Shule ya Msingi Boma ,Esther Abduely wakati akiongea na waandishi wa habari juu ya  maadhimisho ya siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike (IDGC )yanayotarajiwa kufanyika mkoani Dodoma.

Amesema kuna umuhimu wa kuweka mkakati katika kuwawezesha wanawake vijana kuchukua nafasi za uongozi katika sekta mbalimbali ikiwemo shuleni kwani asilimia 68.5 ya wanafunzi  hawajawahi kugombea au kuonesha nia ya kugombea nafasi yoyote ya uongozi kwa ngazi ya shule.

Amesema kati ya hao asilimia 44 hawashiriki katika chaguzi za uongozi wa wanafunzi na katika tafiti hiyo wasichana wako nyuma zaidi kwenye masuala ya mchakato wa uongozi katika nyanja mbalimbali kama vile nyumbani, shuleni na katika jamii.

“Utakuta kama ni nyumbani mtoto wa kiume anashirikishwa na kutoa  mawazo yake kuhusu masuala mbalimbali ya kimaendeo nyumbani,ikiwa mtoto wa kike hapewi nafasi hiyo au anapaswa kuwa msikilizaji tu na mtekelezaji wa maamuzi yanayofanyika,”amesema na kuongeza 

“Katika mazingira ya shule pia wakati mwingine wanafunzi hawapewi nafasi ya kuonesha nia ya kugombea au kuchagua kiongozi  wanayempenda badala yake wanaweza kuchaguliwa kiongozi ambaye anafanya vizuri kitaaluma au ni mkubwa kuliko wote kiumri,”amesema Abduel.

Amesema uchaguzi huo kwa viongozi katika shule unaweza kuwaminya fursa kwa wanafunzi wenye uwezk kuonesha uwezo wao kwa kuongoza au kutumia haki yao ya kuchagua kiongozi wanayempenda.

Akizungumza siku hiyo ya mtoto wa kike mwaka huu,Mmoja wa  Msichana Kiongozi  kutoka Shule ya Sekondari ya Einoti,Angel Mbwambo amesema  mwaka huu ajenda ya msichana itazingatia umuhimu wa wasichana na uongozi katika kuwawezesha wasichana kufikia malengo yao ya uongozi.

Amesema ajenda hiyo inalenga kufungua milango ya fursa kwa wasichana kujifunza,kujielez na kusimamia mabadiliko chanya katika jamii zao.

“Katika kuadhimisha siku hii muhimu mwaka huu wadau wa haki za wasichana kutoka mashirika saba ikiwemo Msichana Initiative, TAI,GLAMI,Flaviana Matata,C-Sema ,Young Mothers Foundation na Wite sawa wameshirikiana katika kuandaa maadhimisho haya yaliyobeba kauli mbiu ya “wasichana na uongozi, kutumia fursa ya teknolojia za kidigitali, “amesema.

Amesema kabla ya kilele hicho wataweza kufanya matukio mbalimbali katika mikoa ya Arusha,Pwani,Morogoro, Dar es Salaam,Mwanza,Tabora ,Dodoma,Mbeya pamoja na Zanzibar  ambapo yatuwakutanisha na wasichana wengine ili kuzungumza masuala mbalimbali yanayohusu kaulimbiu ya mwaka huu.

Naye Mratibu wa Programu kutoka Taasisi ya Flaviana Matata, Brian Terry  amesema kila mmoja  anajukumu la kuhakikisha kuwa anajenga mazingira ambayo yatampa mtoto wa kike nafasi ya kustawi, kujifunza, na kutumia vipaji vyake kikamilifu.

Amesema katika kusherekea maadhimisho hayo wataweza kuwapa elimu ya Uongozi na Tekinologia wasichana hao na  kukusanya maoni yao kwa lengo la kutomuacha mtu nyuma na kuhakikisha sauti za mabinti  zinasikika.