September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mpimbwe yaokoa zaidi ya tani 20 za miti matumizi ya gesi


Na George Mwigulu,Timesmajiraonline,Mpimbwe.

ZAIDI ya tani 22 za miti kila mwezi zinanusurika kukatwa kwa ajili ya matumizi ya kuni za kupikia chakula katika shule ya sekondari ya Mizengo Pinda Mkoani Katavi kutokana shule hiyo kuacha matumizi ya kuni na kuanza kutumia nishati safi yakupikia.

Mwanafunzi wa shule hiyo, Antia Jovin amebainisha hayo kwa Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2024 Godfrey Mnzava September 9, 2024 akimweleza mwaka 2022 wakiwa vijana 50 waliazisha Klabu ya mazingira ili kushinikiza mabadiliko shuleni hapo ya uhifadhi mazigira.

Antia amesema, Shule yao iliyopo katika halmashauri ya Mpimbwe waliona utunzaji wa mazingira ili uweze kufikiwa kwa masirahi ya ujenzi wa taifa endelevu njia pekee ni kutumia nishati safi.

“Matumizi ya nishati safi ya gesi yatanusuru uharibifu wa mazingira” amesisitiza mwanafunzi huyo na mhifadhi wa mazingira akijivunia mafanikio yaliyopatikana kupitia klabu yao ambapo kwa sasa shule hiyo imeondokana na matumizi ya kuni kama nishati ya kupikia.

Ameweka wazi kuwa kupitia klabu, Halmashauri imewawezesha shuleni hapo kupanda miti 5950 ya kivuli na matunda, miti asilia 624 na uanzishaji wa bustani ya miche ya miti ya matunda 300 kama njia nyingine ya kuhakikisha uhifadhi wa mazigira unafanikiwa.

“Matumizi ya nishati gesi ya kupikia tunatambua ni utekelezaji wa maagizo ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ya kutumia nishati safi ili kupunguza au kudhibiti kabisa matumizi ya nishati ya kuni na mkaa nasi tumefanya kupitia halmashauri yetu,”amesema.

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2024, Godfrey Mnzava amesema kuna changamoto ya mabadiliko ya tabia ya nchi inayosababishwa na uharibifu wa mazingira ambapo zaidi ya asilimia 90 yanachangiwa na shughuli za kibinadamu.

Mnzava ameeleza kuwa ongezeko la joto juu ya uso wa dunia, mafuriko na maporomoko, ardhi kupoteza rutuba, majira ya mwaka kubadilika ni sehemu ya athari zinazojitokeza kutokana na uharibifu  wa mazingira.

Kutokana na uanzishwaji wa klabu hiyo amesema ni muhimu kupandikiza mbegu kwa vijana katika masuala  ya utunzaji wa mazingira na matumizi ya nishati safi kwani ni tabia itakayosaidia kuwa na taifa endelevu.

“Kupitia uhifadhi mzuri wa mazingira una tija kwani ndani ya mazingira ndiko kunakopatikana rasilimali zote na maligafi kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli mbalimbali” Amesema Mnzava.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mwanamvua Mrindoko akipokea Mwenge wa Uhuru kutoka Mkoa wa Rukwa amesema kuwa jumla ya miradi 43 itatembelewa na mwenge huo kwa ajili ya kuweka mawe ya msingi na kuzinduliwa yenye thamani ya fedha Bilioni 11.8

Ambapo leo September 9, 2024 tayari Mwenge wa Uhuru ukiwa katika halmashauri ya Mpimbwe umekimbizwa km 232.5 kutembelea miradi ya maendeleo minne yenye thamani ya Bil 4.495, Umeweka mawe ya msingi katika miradi miwili thamani yake ni Mil 628.409 na miradi miwili yenye thamani ya Mil 16.72.

Mwenge wa Uhuru September 10, 2024 utakuwa katika halmashauri ya wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi ambapo utazindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali ya maendeleo.