September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM yawataka wafugaji,wakulima Kiteto kutumia 4r za Rais Samia

Na Agnes Alcardo,TimesmajiraOnline,Kiteto

KATIBU wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Taifa,CPA Amos Makalla,amewataka wafugaji na wakulima wa Wilaya ya Kiteto Mkoani Manyara kuacha kuwa na migogoro ya ardhi na badala yake watumie 4r Za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

CPA Makalla amesema hayo leo Septemba 9, 2024 akiwa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kata ya Engisero, akisema Tanzania ni nchi yenye amani na upendo hivyo ni vyema jamii hizo mbili zikaishi kwa maridhiano ili kukomesha migogoro ya ardhi inayotokea mara kwa mara na kusababisha Hali ya uvunjifu wa amani

Aidha amekemea vitendo vya baadhi ya wananchi kuvamia maeneo na kusema kuwa, Serikali itahakikisha maeneo hayo yanafanyiwa tathimin, huku akisisitiza kuwa nia ya serikali ni nzuri na yenye kuleta maendeleo kwa Taifa.

Pia amesema, wapo viongozi ambao hawakubaliki katika jamii ikiwemo kutotatua kero za wananchi na kutosoma taarifa za mapato na matumizi.

“Niwaombe ndugu zangu muendelee kukiamini chama cha mapinduzi na kukipa kura nyingi katika uchaguzi wa serikali za mitaa na tunawaahidi kuwaletea wagombea wanaokubalika na wananchi na siyo mgombea mpaka umsafishe na dodoki sisi muda huo hatuna”, amesema Makalla.

Pia amewataka wananchi kwenda kujiandikisha kwenye daftari la makazi Octoba 12 hadi 20 mwaka huu tayari kwa ajili ya kupiga kura.

“Tujitokeze kwa wingi ndani ya hizo siku 10 kwenda kujiandikisha kwenye daftari la makazi ili tuweze kushiriki kupiga kura katika ucbaguzi wa serikali za mitaa kwani kitambulisho pekee katika uchaguzi huu hakitoshi”, ameongeza.

Aidha ameongeza kuwa,CCM itahakikisha uchaguzi wa Serikali za Mitaa unafanyika kwa amani, utulivu na haki, huku akisema kuwa matokea ya uchaguzi yatatangazwa kwa uwazi na haki.

“Mshindi atatangazwa kwa uwazi na atatangazwa atakaye kuwa na kura nyingi na si vinginevyo” amesema