September 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM haihusiki na kauli ya aliyekuwa DC Longido

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online. Arusha

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema hakihusiki na kauli iliyotolewa na aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Longida, Marco Ng’umbi, uliyosema kuwa ushindi wa Madiwani wa CCM katika Wilaya hiyo wa mwaka 2020 haukutokana na nguvu zao bali ulitokana na mpango ulikuwa umesukwa na Serikali.

Kauli hiyo, imetolewa leo Septemba 4, 2024 na Katibu wa NEC, Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM Taifa, CPA Amos Makalla, Jijini Arusha alipokutana na viongozi wa CCM wa Mkoa huo pamoja na Wakuu wa Taasisi za Serikali zilizopo katika mkoa huo.

Makalla alisema,maneno aliyoyasema Ngumbi hayahusiani na CCM na kudai kuwa hayo ni maneno yake binafsi huku akiwataka viongozi kuwa na utaratibu wa kuandaa hotuba zao kabla ya kufanya mikutano ili kutoleta sintofahamu katika jamii.

“Mimi ndiyo mwenezi wa CCM hivyo nasema kuwa, hayo aliyosema huyo aliyekuwa Mkuu w a Wilaya ya Longido sisi kama CCM hayatuhusu kwani anaonekana aliishiwa hotuba akawa anatafuta maneno yake mwenyewe na ndiyo maana viongozi wa namna hiyo hatuwataki.

Niwaombe na viongozi wengine kuwa na utaratibu wa kupanga hotuba vizuri na siyo kutengeneza sinema na maneno ya ajabu kama ya huyu aliyekuwa porini na sisi hatujui alienda huko kufanya Nini kama alienda kuchimba dawa au kufanya chochote sisi hayatuhusu lakini itambulikr kuwa sisi hatukumtuma kwa Yale aliyosema huyo achukuliwe kama mtu aliyeishiwa hotuba. Amesema Makalla.

Pia, amewaagiza Wenyeviti wa CCM katika Wilaya zote nchini, kutokubali kuingiliwa wakati wa vikao vya Halmashauri kuu za wilaya kuteua majina ya wagombea wa nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa serikali za Mitaa na baadhi ya watu wanaopanga safu zao za kuwasaidia katika ya Uchaguzi Mkuu wa mwakani.

” Wenyeviti simamieni dhamana tuliyowapa ya kuteua majina ya wagombea safi watakao tuwakilisha kugombea nafasi mbalimbali katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa na msikubali kuteua wagombea kwa kuletewa vimemo na watu kwa sababu mtatuoa kazi ya kuwasafisha kwa madodoki na sisi muda huo hatuna” ameongeza Makalla.

Katika hatua nyingine CPA Makalla alisema CCM inaheshimu 4R za Rais Dk,Samia kwa sababu hiyo hatafanya ziara katika wilaya Ngorongoro kutokana na katazo lililotolewa na jeshi la Polisi.

“CCM ni chama Tawala ndicho chenye serikali tungekuwa na uwezo wa kuishinikiza tukafanye ziara katika wilaya ya Ngorongoro lakini kwa kuwa tunaheshimu 4R za Rais Dk Samia tumeheshimu na hatutakwenda Ngorongoro vyama vingine vya siasa ili liwe funzo kwao wanapokatazwa kwenda mahali wasilamike”, amesema.