September 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CHAUMMA wamuomba Rais Samia kuingilia kati suala la wakulima wa Mbaazi Kondoa

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma

CHAMA Cha Ukombozi wa Umma(CHAUMMA)kimemuomba Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kuingilia kati suala la kukamatwa kwa magari yaliyobeba zao la Mbaazi na Ndegu mali ya wakulima wa Wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma kwa vigezo vya stakabadhi ghalani.

Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho,Kayumbo Kabutari amezungumza na waandiahi wa habari jijini hapa leo,Septemba 4,2024
ambapo amedai kuwa Serikali ya Mkoa wa Dodoma imeendesha zoezi la unyang’anyi wa mazao kwa wakulima hao kwa kigezo cha stakabadhi ghalani.

“Sasa jambo hili limekuwa likiwaumiza sana wakulima kwani serikali ya mkoa wa Dodoma imekuwa ikipora na kunyang’anya mazao ya wakulima bila kuangalia athari inayomkuta mkulima na kweli lipo neno stakabadhi ghalani lakini lina utaratibu wake,”amesema Kibutari.

Amefafanua kuwa sheria na.10 ya mwaka 2005 na sheria na.3 ya mwaka 2015 na marekebisho yake ya mwaka 2016 juu ya stakabadhi ghalani imeweka mambo vizuri kabisa ambapo amesema stakabadhi ghalani inaendana sambamba na uanzishaji wa vyama vya ushirika vya wakulima ambapo Dodoma hakuna.

“Sasa leo unapoenda kumuanzishia mtu ghafla aliyehangaika toka kuandaa shamba lake yuko peke yake kazi zote za shamba anazifanya mkulima peke yake kwenye mazao unakuja kumwambia kuna kitu kinaitwa stakabadhi ghalani inakuwa siyo sawa,”amesema Kibutari.

Amesema kuwa lengo la stakabadhi ghalani ni kwajili ya kumsaidia mkulima asipatwe bei ya dira bei ambayo ya mtaani kwamba wanamuanzishia hizi stakabadhi ghalani ili mkulima aweze kunufaika na bei nzuri itakayopatikana.

“Lakini kabla hujafika kwa mkulima lazima awe amewezeshwa kwani moja ya kazi za stakabadhi ghalani ni kusimamia na kuhamasisha matumizi ya mfumo wa stakabadhi ghalani jambo hili serikali ya mkoa wa Dodoma haijafanya.

“Nakatika kusimamia huku kuendane sambamba na uwepo wa vyama vya ushirika visipofanyika hivyo kinachofanyika ni kwenda kuwapora wananchi mazao yao kitu ambacho siyo lengo wala dhamira ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan ambaye lengo lake kubwa ni kutaka kuwainua wakulima kwenye kilimo siyo kuwakandamiza.,”amesisitiza.

Na Kuongeza “Mfano tarehe 27 mwezi wa nane mwaka huu wakulima wa mbaazi wakiwa wametoka na gari 14 zikiwa na tani zaidi ya 150 zikitoka Kondoa zikiwa na Mazao ya Mbaazi gari 11 na dengu gari 3 wakiwa wametoka Halmashauri ya Kondoa kuchukua ushuru wa hayo mazao wanaleta mjini sokoni na Kondoa hakuna chama cha ushirika wa kukusanya hayo mazao na wanalipa ushuru wa hayo mazao wanaleta sokoni Dodoma mjini wanafika Chemba wakulima wanakamatwa wanaambiwa stakabadhi ghalani.

“Magari yazuiliwa ambapo siku hiyo bei ya soko ilikuwa kilo moja ya mbaazi ilikuwa 2060 lakini yakazuiliwa Chemba na wanatoka Kondoa Halmashauri nyingine wanafika Halmashauri nyingine wanazuiliwa waambiwa stakabadhi ghalani,kwanini haikuanzia walipotoka ili wakulima waufahamu na kwanini Halmashauri ya Kondoa isiwazuie wakulima kutoka kondoa,”amesema.

Tarehe 2 mwezi wa 9 kuna mnada umefanyika Chemba kilo imeuzwa kwa 1840 tofauti na bei waliyokuwa wanaitarajia ya 2060 na hawajawalipa wakulima.

“Stakabadhi ghalani inasema pale mnunuzi anapopatikana anatakiwa kulipa pesa yote palepale na mkulima anatakiwa apewe haki yake lakini hadi sasa toka tarehe 2 Septemba mnada umefanyika kwa kilo 1840 badala ya bei waliyokuwa wanaifukuzia ya kilo 2060 mpaka leo mkulima hajapewa hela yake na amekodi gari kuleta mzigo mjini na amlipe mwenye gari huu ni unyanyasaji,”

Aidha ameitaka Serikali ya mkoa wa dodoma wajipange kwabi amedai wanamharibia Rais kazi yake kwani mfumo wa stakabadhi ghalani unaendana na vyama vya ushirika na kanuni inasema katika mfumo wa stakabadhi ghalani malipo yanafanyika katika chama kikuu cha ushirika hayafanyiki kwenye vyama vya msingi na Dodoma hakuna chama cha ushirika.

Naye Mkulima kutoka Wilaya ya Kondoa, Zabibu Yusufu amesema kuwa wao kama wakulima wamaepata hasara kubwa kwani wametoka Kondoa na mazao wanazuiwa Chemba toka tarehe 27 mwezi wa nane hadi tarehe 2 mwezi wa tisa ambapo waliuza kwa 1840 badala ya 2060 waliyokuwa wanatarajia kuuza kwa siku hiyo

“Zile gari zimekamatwa zikiwa na tani 180 wale wakulima wote zile gari 14 kunawakulima ambao tayari wameshapewa mitaji na wanunuzi ili waweze kulima wapate mazao waje wawauzie wale waliowapa mitaji lakini kuna wengine wamekopa benki na wengine wamekodi gari hawajalipia wengine wanawagonjwa wanawatoto wanataka ada tumeathirka vikubwa,”amesema Yusufu.

Ameongoza “Na kunawengine wamepigwa kuna kijana mmoja hadi amelazwa kwa kupigwa kwa kosa tu la kuchukua picha wakati magari tanakamatwa na kunawengine wamebeba mazao kwa malikauli kule vijijini kwasababu mbaazi kwa mkoa wa Dodoma asilimia kubwa wanaolima mbaazi ni Kondoa vijijini lakini wamezuiliwa Chemba ni hasara.

“Tunaiomba Serikali kama kunakitu wanataka wakifanye hukusu stakabadhi ghalani wasibuni buni njia za kuwakandamiza wakulima,Mhe.Rais na Waziri wa Kilimo waangalie hili vyama vya ushirika katika mkoa wa Dodoma kwamba kwa wakulima wafanyenini ili vyama ushirika vianzishwe viwaunganishe wakulima.