September 22, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NaCoNGO watakiwa kutumia mafunzo kufuata maadili

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum Felister Mdemu  ameyataka mashirika yasiyo ya kiserikali kuendelea kufuata sheria na kanuni hasa katika utumiaji wa taarifa za utekelezaji na ulipaji ada.

Naibu Katibu Mkuu huyo ametoa kauli hiyo wakati akizungumza katika ufunguzi wa Mafunzo Ya Wajumbe Wa Baraza la Taifa Mashirika yasiyo ya Kiserikali (NaCoNGO) na Wasajili Wasaidizi yaliyofanyika jijini  Dodoma katika ukumbi wa  Mikutano wa Jakaya Kikwete.

Amesema mafunzo hayo yalioyoandaliwa na Wizara hiyo kupitia Ofisi ya Msajili wa NGOs kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani , yawe chachu kwao katika  kufuata sheria na kanuni na hivyo kuongeza uwazi na tija katika utendaji kazi wao.

“Wizara inatarajia baada ya Mafunzo haya mtakuwa na ufanisi katika utendaji kazi wenu katika uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali,

“Hii itasaidia Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kuzingatia Sheria katika utendaji kazi wake ikiwa ni pamoja na ulipaji wa ada, utumaji wa taarifa na mikataba ya fedha.”amesema  Mdemu

Ameongeza kuwa “aidha, tunatarajia kutaongezeka kwa uwazi na uwajibikaji wa shughuli za Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na yatajikita katika kuzingatiaji mila na desturi za mtanzania na kuhakikisha miradi inayotekelezwa inanufaisha jamii inayolengwa ili kuleta maendeleo kwa jamii na Taifa kwa ujumla.”

Hata hivyo Mdemu amesema kuwa, Wizara inatambua kuwa kuna changamoto mbalimbali katika uratibu kamavile, ukosefu wa mafunzo ya mara kwa mara kuhusu Sheria, Kanuni na Miongozo ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, mafunzo ya mfumo wa Kieletroniki wa usajili na uratibu (NIS), na ufinyu wa bajeti ya kufanya ufuatiliaji wa shughuli za Mashirika Yasiyo ya Kiserikali.

“Kwa hiyo , Wizara imeamua kuandaa mafunzo haya ili kuwapitisha katika Sheria,Kanuni na Miongozo, mfumo wa Kieletroniki wa usajili na uratibu (NIS) maana mfumo huu umefanyiwa mabadiliko hasa baada ya kuongezewa kipengele cha Ramani ya Kidigitali. “amesema

Aidha amesema, kutokana kuboreshwa kwa mfumo wa Kieletroniki wa usajili na uratibu (NIS) baadhi ya taarifa zitahitajika kuhuishwa katika mfumo huo.

Amesema,taarifa za Mashirika katika maeneo yao zinahitajika kuhuishwa na kuingiza taarifa za Vikundi vya kijamii (CBOs) katika mfumo huo.

Awali Mwenyekiti wa Baraza la Mashirika Yasiyo ya Serikali (NaCONGO) Makala Jasper ameishukuru Wizara kwa ushirikiano inaotoa kwa mashirika yote nchini katika ngazi zote.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Uratibu wa Mashirika hayo Mwantumu Mahiza amewataka Wasajili kufanya kazi kwa karibu na NGOs kwenye maeneo yao na kufuatilia shughuli wanazofanya kwa mustakabali wa nchi ya Tanzania.