October 9, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Machifu waiomba serikali kuwarejeshea misitu ya asili

Na Esther Macha, TimesmajiraOnline, Mbeya

KIONGOZI wa Machifu Mkoa wa
Mbeya Chifu Rocket Mwashinga ameiomba Serikali kuwarejeshea maeneo ya
misitu ya asili wayatunze ndani ya miaka mitano ili warejeshe uoto wa asili uliopotea kutokana na uhalibifu wa mazingira katika maeneo  mbalimbali hapa nchini .

Chifu Mwashinga amesema hayo Agosti 31,2024 wakati wa hitimisho la mashindano ya mapishi ya chakula kwa Mama Lishe na Baba 1000 kutoka kata 36 Jijini Mbeya ambalo limeandaliwa na Taasisi ya Tulia Trust iliyopo chini ya Spika wa Bunge na Mbunge wa Jimbo la Mbeya mjini na Rais umoja wa Mabunge Duniani (IPU)mbaye pia ni Mkurugenzi Taasisi hiyo.

“Serikali ituwezeshe sisi machifu kulinda mazingira kwani tuna uwezo mkubwa sana na tukisimama imara na kurudisha uoto wa asili na utunzaji mazingira utakuwa vizuri katika maeneo yote “amesema Chifu Mwashinga.

Amesema kuna kipindi akiwa Dodoma alizungumzia ndani ya miaka 10 machifu wote wakishirikiana kulinda mazingira nchi itakuwa kijani na kuomba nishati ya gesi waliyoleta ipungue bei ili  kuendelea kuokoa mazingira.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga ameipongeza Taasisi ya Tulia Trust kwa kuendelea kuleta tija kwa Mama lishe na Baba Lishe wa Mkoa wa Mbeya katika shughuli zao na kuwajenga kiuchumi pamoja na jitihada za kutunza mazingira.

Kapinga amesema Tamasha hilo ni mwendelezo wa jitihada za serikali  ya awamu ya sita katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia na serikali imeandaa mkakati wa kufikia zaidi ya asilimia 80 wawe wanatumia nishati safi ya kupikia na  inaendelea na kampeni  ili kuhakikisha inawafikia watanzania wengi zaidi.

Hata hivyo Kapinga ameeleza kuwa mwaka 2023 ilianza kutoa Ruzuku ya mitungi ya gesi ambapo mwaka uliopita walitoa mitungi ya gesi 104,000 .

Kwa upande wake Shekhe wa msikiti wa Isanga,Ibrahim Bombo amesema kuwa kama viongozi wa dini wataendelea kushirikiana na Dkt.Tulia katika kulinda na kutunza mazingira kwa kuhamasisha matumizi Bora  ya nishati safi ya Gesi.