September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali kupeleka umeme vitongoji 15 kila Jimbo

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma.

NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dkt. Doto Biteko ameshuhudia utiaji saini mikataba ya kupeleka umeme kwenye vitongoji 15 kwa kila jimbo huku akiuagiza wakala wa Nishati Vijijini kuwasimamia wakandarasi katika utekelezaji wa miradi hiyo ili iweze kukamilika kwa wakati na kwa kiwango chenye ubora.

Pia ametoa onyo kwa wakandarasi wanaowauzia nguzo za umeme wananchi pindi wanapotaka kupatiwa huduma hiyo.

Akizungumza katika hafla hiyo ya utoaji saini wa mkataba ya kupeleka umeme kwenye vijiji hivyo ,Dkt.Biteko amesema kuwa ,ni jukumu la REA kuhakikisha wanawasimamia wakandarasi katika shughuli hiyo.

Aidha ameitataka REA kuona changamoto kabla ya mradi kuanza ili kuepusha kusuasua kwa miradi hiyo.

“REA mnatakiwa kutambua changamoto za eneo husika kabla ya mradi kuanza kwani itasaidia kuondoa kusuasua kwa mradi,kumekuwa na kesi nyingi kwamba eneo hili lilikuwa na changamoto fulani sasa inabidi mtambue changamoto hizo mapema kabla kuanza kwa mradi huo,”amesema

Ameongeza “kumekuwa na tabia ya baadhi ya wakandarasi kuwauzia nguzo wateja wanapotaka kuvutiwa umeme,sitalifumbia macho suala hili wakandarasi fanyeni kazi kwa kufuata weledi na maadili nasio kukiuka maadili ya kazi zenu tabia ya kuwauzia nguzo wananchi haitakiwi kabisa wapatieni huduma watanzania,”

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu REA Mhandisi Hassan Said amesema kuwa Mpango wa Serikali kupitia Wakala ni kufikisha umeme kwenye vitongoji 13,000 katika miaka mitatu ijayo, tukianza na vitongoji 3,060 ambavyo mikataba ya utekelezaji wa mradi wa kupeleka umeme katika vitongoji hivyo inasainiwa leo.

Amesema kuwa Hatua hiyo itafanya asilimia 71 ya vitongoji vyote Nchini kufikiwa na huduma za umeme ifikapo mwaka 2028/29.

“Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mikataba inayosainiwa leo ni ya mradi wa kupeleka umeme katika vitongoji 3,060 ikiwa ni vitongoji 15 kwa kila Jimbo katika majimbo 204 ya uchaguzi yaliyopo katika mikoa 25 ya Tanzania Bara isipokuwa mkoa wa Dar es salaam,

Utekelezaji wa mradi huu utakuwa katika mafungu 25 katika mikoa 25 ya Tanzania Bara, ambapo kutokana na sababu za kimanunuzi mafungu 23 yalipata wakandarasi isipokuwa mikoa ya Singida na Tanga, ambayo zabuni yake itatangazwa tarehe 22 Agosti 2024,”alisema.

Aidema kuwa Mikataba inayosainiwa itahusisha ujenzi wa njia za msongo wa kati wa umeme zenye urefu wa km258, ujenzi wa njia za msongo mdogo wa umeme zenye urefu wa km6118, ufungaji transfoma 3,059 pamoja na kuunganisha wateja takribani laki moja (100,000), hatua ambayo itaongeza uunganishwaji wa wananchi na huduma za umeme (connectivity) kwa gharama za takribani Bilioni 360.

“Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, utekelezaji wa mradi huu utaongeza mtandao wa njia za umeme kwenye vitongoji na hivyo kuwezesha upatikanaji wa umeme kwenye maeneo yenye shughuli za kijamii zikiwemo shule, zahanati na maeneo ya biashara,

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) ulianzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Nishati Vijijini Na. 8 ya Mwaka 2005 na kuanza kazi rasmi Mwezi Oktoba 2007, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa iliyokua Sera ya Taifa ya Nishati ya Mwaka 2003.

Lengo kuu la Wakala ni kuhamasisha na kuwezesha upatikanaji wa nishati bora maeneo ya vijijini,Katika kulifikia lengo hilo, Wakala umekuwa ukitekeleza miradi mbalimbali ambapo tangu kuanzishwa kwake takribani vijiji 12,167 kati ya 12,318 sawa na asilimia 98.8 vimeshapatiwa umeme.