September 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia atunukiwa tuzo ya ustahamilivu na mabadiliko ya PSSSF

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online


RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametunukiwa tuzo ya Ustahamilivu na Mabadiliko ya Miaka Mitano ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) jijini Dodoma Agosti 12, 2023.

Tuzo hiyo imepokelewa na Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa kwa niaba ya Mhe. Rais, wakati wa hafla ya kuadhimisha miaka mitano tangu kuanzishwa kwa PSSSF, kufuatia uamuzi wa Serikali wa kuunganisha Mifuko minne ya Hifadhi ya Jamii ya PSPF, PPF, LAPF na GEPF, Agosti, 2018.

Akieleza sababu za Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kukabidhiwa tuzo hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mhe. Profesa Joyce Ndalichako, ambaye alikabidhi tuzo hiyo kwa niaba ya PSSSF, alisema, Dkt. Samia ni sehemu ya Mabadiliko hayo yaliyopelekea ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Mfuko.

“Tunamshukuru kwa dhati, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake ya dhati kuhakikisha kwamba wastaafu wa nchi hii hawapati usumbufu na hivyo kutoa fedha kiasi cha shilingi trilioni 2.7 katika mfumo wa hati fungani ambazo kwa hakika zimeimarisha sana uwezo wa Mfuko kuwahudumia Wanachama wakiwemo Wastaafu katika ulipaji wa Mafao kwa wakati.” Alifafanua.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF)  CPA. Hosea Kashimba amesema kuwa katika kipindi cha miaka mitano, hadi kufikia Juni, 2023 mfuko huo umelipa kiasi cha shilingi trilioni 8.88 kwa wanufaika 262,095.

Amesema kuwa kati ya Julai, 2018 na Juni, 2023 mfuko huo umeweza kulinda na kuongeza thamani yake kwa asilimia 27.76 kutoka trilioni 5.83 hadi trilioni 8.07 Juni, 2023. “Ongezeko hili ni sawa na wastani wa asilimia 6.72 kwa kila mwaka”.

“Mhe. Waziri Mkuu, hivi sasa kila mwezi tunalipa shilingi bilioni 67 kama pensheni kwa wanufaika 164,828 na tunalipa kila ifikapo tarehe 25 ya mwezi husika bila kuchelewa.” Alifafanua CP. Kashimba.

Na sasa Mfuko unalipa Mafao ndani ya siku 60 kwa mujibu wa sheria, alisisitiza CPA. Kashimba.

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa (katikati), akionesha tuzo ya Ustahimilivu na Mabadiliko ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishiwa Umma (PSSSF) aliyotunukiwa Mhe. Dkt. Samua Sukuhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa hafla ya kutimiza miaka mitano tangu kuanzishwa kwa PSSSF jijini Dodoma Agosti 12, 2023. Wengine pichani ni Mhe. Profesa Joyce Ndalichako (kushoto), Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) na Mhandisi Mussa Iyombe, Mwenyekiti wa Bodi ya Wdhamini PSSSF.

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa (katikati), akionesha tuzo ya Ustahimilivu na Mabadiliko ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishiwa Umma (PSSSF) aliyotunukiwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakati wa hafla ya kutimiza miaka mitano tangu kuanzishwa kwa PSSSF, jijini Dodoma Agosti 12, 2023. Wengine pichani ni Mhe. Profesa Joyce Ndalichako (watatu kushoto), Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii,  Mhe. Fatma Yawfiq (wapili kushoto), Rais wa TUCTA, Bw. Tumaini Nyamhokya (wakwanza kushoto), Mwenyekiti wa Bodia ya Wadhamini PSSSF, Mhandisi Mussa Iyombe (watatu kulia), Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule (wakwanza kulia) na Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, CPA. Hosea Kashimba (wapili kulia) 

Wakurugenzi Wakuu wastaafu wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii iliyounganishwa na kuunda PSSSF

Baadhi ya Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini PSSSF.