October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Rais Dkt. John Pombe Magufuli akikabidhiwa Fomu ya kuomba ridhaa ya kuteuliwa kugombea Urais kwa Tiketi ya CCM katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika baadae mwaka huu kutoka kwa Katibu Mkuu wa CCM Dkt. Bashiru Ally Kakurwa katika Ofisi za Makao Makuu ya CCM White House Dodoma leo tarehe 17 JUNI 2020.

Kumekucha, Rais Magufuli achukua fomu kuwania Urais

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

RAIS John Magufuli, amechukua fomu ya kuomba kusimamishwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwania Urais katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Rais Magufuli amechukua fomu ya kuwania urais Makao Makuu ya CCM jijini Dodoma muda mfupi uliopita ambayo amekabidhiwa na Katibu Mkuu wa CCM, Dkt. Bashiru Ally.

“Nimeishachukua fomu, kwa hiyo nitaanza kutafuta wadhamini wa hapa hapa Dodoma,” amesema Rais Magufuli wakati akizungumza na wana-CCM walijitokeza kwa ajili ya kushuhudia tukio hilo.

Mara baada ya kuchukua fomu alipokuwa akiondoka, Rais Magufuli amekutana na makada wa Chama hicho waliokuwa wamejawa furaha, huku mmoja wao akimpa pole kwa kuuguliwa na mama yake.

Makada hao wa CCM wamemhakikishi Rais Magufuli kwamba ni makada wa Chama hicho na wapo tayari kumdhamini. Katika kinyang’anyiro hicho ndani ya CCM, Rais Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa CCM Taifa, hatarajiwi kupata upinzani kutokana na mila na desturi za chama hicho kuachiana muda ili Rais anayekuwa madarakani amalize kipindi chake cha miaka kumi ya uongozi wake.

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Rais Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na wanachama wa CCM katika Makao Makuu ya CCM White House Dodoma leo tarehe 17 JUNI 2020 mara baada ya kuchukua Fomu ya kuomba kuteuliwa kugombea nafasi ya Urais kwa Tiketi ya CCM katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika baadae mwaka huu.

Rais Magufuli amechukua fomu ili kuomba kusimamishwa na CCM kuwania muhula wa pili wa uongozi wake ambao akiumaliza atakuwa amehitimisha ngwe ya miaka 10 ya Serikali ya Awamu ya Tano.

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM Rais Dkt. John Pombe Magufuli akitoka katika Ofisi ya CCM Makao Makuu ya Mkoa Dodoma mara baada ya kupata wadhamini wa Chama chake cha Mapinduzi CCM. PICHA NA IKULU