October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

UWAST yalaani waliopanga kuandamana jana

Na Rose Itono,TimesMajira Online.

UMOJA wa Wanaharakati Siasa Tanzania (UWAST), umesema unalaani vikali baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani ambavyo vilipanga kufanyika maandano nchi nzima kupinga Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 28 mwaka huu, ambayo hata hayakufanikiwa.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana Kiongozi Mkuu wa Umoja huo, Kunje Ngombale Mwiru amesema baadhi viongozi wa vyama hivyo waliopanga maandamano hayo hawaitakii mema Tanzania.

Amesema wao kama UWAST wajumbe wake wote wanatoka katika vyama mbalimbali vya siasa nchini, hivyo wanatoa tamko hilo wakiwa wamekubaliana kwa dhati.

Ngombale amesema vyama vya upinzani vinatakiwa kukubali matokeo na kukaa chini kujipanga upya kwa kuwa kukiondoa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ni kazi kubwa kuwa ni chama ambacho kimeota mizizi na kimejipanga kwa muda mrefu.

“Chama hakiwezi kutaka kuongoza nchi wakati hakina hata Mjumbe wa Nyumba Kumi, huwezi kushindana na CCM ambayo ina uzoefu wa muda mrefu katika kuongoza nchi, hivyo ni lazima wapinzani wajipange kisawasawa,” amesema.

Ngombale ambaye katika uchaguzi huo aligombea Ubunge Jimbo la Kibaha kupitia Chama cha Sauti Umma (SAU), amesema wao kama wanaharakati wanaunga mkono uchaguzi wa mwaka huu kwa kuwa ulikuwa huru na wa haki.

Amesema anaipongeza Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), serikali pamoja na Jeshi la Polisi kwa kufanikisha uchaguzi uliofanyika kwa amani, huru na haki.