March 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali kujenga bwawa la mil.480 Liwale

Na Mbaraka Kambona,TimesMajira Online,Liwale

NAIBU Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amesema katika bajeti ya mwaka 2021/2022 Serikali itajenga bwawa la kunyweshea Mifugo lenye thamani ya Shilingi Milioni 480 katika Kijiji cha Kimambi, Wilayani Liwale, Mkoani Lindi.

Ulega ameyasema hayo juzialipofanya ziara katika Wilaya ya Liwale, Mkoani Lindi kwa lengo la kusikiliza kero za Wafugaji na Wakulima ili kuzitatua.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega (katikati) akitoa maelekezo kwa Mkuu wa Wilaya ya Liwale, Judith Nguli (kulia) alipotembelea kukagua eneo lililotengwa kwa ajili ya kujengwa bwawa la kunyweshea Mifugo katika Kijiji cha Kimambi, Wilayani Liwale, Mkoani Lindi Septemba 20, 2021.

Amesema ujenzi wa bwawa hilo utasaidia kutatua changamoto ya maji ambayo inawakabili wafugaji wa maeneo hayo na utasaidia pia kutatua migogoro baina yao na wakulima Wilayani humo.

“Rais Samia Suluhu Hassan anakwenda kuwajengea bwawa lenye thamani ya Shilingi Milioni 480 hapa Kimambi, ujenzi wa bwawa hilo utasaidia kuwaondosha katika migogoro,” amesema Ulega.

Naibu Waziri Ulega alisisitiza kuwa pesa hizo zipelekwe kufanya kazi iliyopangiwa ya ujenzi wa bwawa la kunyweshea mifugo huku akiwataka viongozi wa Wilaya hiyo kuhakikisha pesa hizo zinatumika vizuri.

Aidha, amesema kuwa Rais Samia Suluhu Hassan amewapa pia Majosho mawili katika Kijiji cha Kimambi na Kijiji cha Luwele.

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega akiongea na Wafugaji na Wakulima wa Kijiji cha Kimambi, Wilayani Liwale, Mkoani Lindi (hawapo pichani) alipofanya ziara katika Wilaya hiyo Septemba 20, 2021 kwa lengo la kutatua kero zao. Katika ziara hiyo Ulega alisema Serikali itajenga bwawa la kunyweshea Mifugo Kijijini hapo lenye thamani ya Shilingi Milioni 480. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Liwale, Judith Nguli.

“Sasa kwa sababu huku mifugo imekuwa mingi sana, Mimi nakuongezeeni Josho lingine hapa ili mifugo mingi iweze kuogeshwa ,”ameongeza Ulega

Naye, Mbunge wa Liwale, Zuberi Kuchauka ametumia nafasi hiyo kumshukuru Rais wa Awamu ya Sita, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuwapelekea pesa hizo huku akisema kuwa bwawa hilo likikamilika hawatarajii tena kuona migogoro katika Vijiji vilivyotengwa kwa ajili ya Wafugaji Wilayani humo.