March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NMB yakabidhi Milioni 60 Maonyesho ya Nanenane – Mbeya

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

Benki ya NMB imeendelea kuiunga mkono serikali katika kufanikisha maonyesho ya Sikukuu ya Wakulima Kitaifa (Nanenane) kwa kukabidhi Sh. milioni 60 kwa ajili ya maonyesho hayo.

Katika hafla ya kukabidhi hundi ya fedha hizo iliyofanyika jana mjini Mbeya, Meneja wa NMB Kanda ya Kusini- Straton Chilongola alisema kuwa benki hiyo imetoa kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kufanikisha shughuli mbalimbali za maonyesho hayo.

Alisema kuwa katika kipindi cha miaka mitano ambayo maonyesho ya Nane nane yamekuwa yakifanyika, NMB imetoa udhamini wa zaidi ya Shilingi milioni 195 katika kufanikisha maonyesho hayo muhimu kwa Taifa.

Chilongola, aliongeza kuwa katika kuunga mkono juhudi za Rais wa Awamu ya sita, Samia Suluhu Hassan, Mchango wa NMB ni kujenga uchumi imara kupitia kilimo na ufugaji ndani ya miaka minne kwani zaidi ya akaunti 644,034 za wakulima zimefunguliwa nchi nzima.

Benki ya NMB inawakaribisha Wananchi wote kutembelea banda lao katika Maonyesho ya Nanenane 2022 ndani ya Uwanja wa John Mwakangale mkoani Mbeya kupata masuluhisho yote ya kifedha.

Mkuu wa wilaya ya Mbeya, Mhe. Dkt Rashid Mohamed Chuachua akipokea mfano wa hundi ya Shilingi Milioni 60 kutoka Meneja wa Benki ya NMB Kanda Nyanda za Juu – Straton Chilongola akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, ikiwa ni sapoti ya kuwezesha maonesho ya Nane Nane yanayofanyika Kitaifa Mkoani Mbeya mwaka huu 2022.