April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mila potofu zachangia ongezeko la vifo vya watoto wanaozaliwa kabla ya wakati

Na Esther Macha, Timesmajira, Online, Mbeya

WANAWAKE wametakiwa kuachana na mila potofu pindi wanapojifungua watoto njiti kwani imani hizo zimekuwa zikichangia ongozeko la vifo vya watoto wachanga wanaozaliwa kabla ya wakati.

Kauli hiyo imetolewa leo na Wakili wa wa Serikali na Mkuu wa Kitengo cha huduma na sheria Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya Mh. Lugano Mwakilasa wakati wa maadhimisho ya siku ya mtoto Njiti duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya.

Mwakilasa amesema kuwa pamoja na sababu zilizoelezwa na watalaam ambazo zinapelekea wanawake walio wengi kujifungua watoto Njiti pia kuwa na imani potofu kwa jamii pindi mama anapojifungua mtoto njiti kumekuwa na imani za kishirikina pindi wanawake wanapojifungua watoto njiti.

Hata hivyo Wakili huyo amewashauri wanawake wajawazito kuhudhuria klink mara wanapojitambua kuwa ni wajawazito ili kuweza kutambua mapema uwepo wa visababishi vya kujifungua mtoto kabla mimba kabla kufikisha wiki 37 na kupata tiba sahihi.

Aidha Mwakilasa amesema kuwa hiyo itasaidia kupunguza sababu mbalimbali zinapelekea mama kujifungua mtoto Njiti.

Hata hivyo Wakili huyo wa Serikali ametoa wito kwa watalaam kuendelea kutoa Elimu kwa jamii kuhusiana na wanawake kuhudhuria klink mara anapojitambua kuwa ni mjamzito ili kugundua visababishi na kupata tiba sahihi.

Akizungumza katika maadhimisho hayo Mkuu wa Idara ya watoto Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya, Dkt. Nuru Mniwa amesema kuwa visababishi vinavyochangia kupata watoto njiti ni pamoja na lishe duni, matumizi ya vilevi kama Pombe, madawa ya kulevya, kifaa cha mimba, maambukizi kwenye kwenye njaa uzazi ambayo ni magonjwa ya zinaa.

Akielezea zaidi Dkt. Mniwa amesema kuwa visababishi vingine ni maambukizi kwenye njia ya mkojo ambayo ni UTI mimba zaidi ya mtoto mmoja, mimba kwenye umri mdogo chini ya miaka 19 na umri mkubwa zaidi ya miaka 35 na msongo wa mawazo wakati wa mimba.

Akizungumza na gazeti hili mmoja wanawake ambaye amewahi kujifungua mtoto njiti, Nikumwita Kajage amesema kuwa aliwahi kujifungua mtoto njiti na kukua vizur na yupo vizur mpaka Sasa kutokana na huduma nzuri aliyopatiwa na madaktari na watoa huduma ambapo mtoto wake alizaliwa chini ya wiki 37 za mimba.

Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya kitengo cha watoto njiti wamesherekea maadhimisho hayo ya siku ya mtoto mtoto njiti Duniani pamoja na wazazi waliowashikisha kujifungua watoto njiti pamoja na wananchi huku Kauli mbiu ikiwa kumbatio la mzazi ni tiba yenye nguvu, muweke mtoto njiti kifuani mwa mama mara tu anapozaliwa.